Header Ads

ABDI BANDA ASIMAMISHWA SIMBA, KUTOCHEZA MECHI MBILI - TFF

Beki wa kushoto wa timu ya Simba, Abdi Banda, amesema kuwa amefungiwa mechi mbili na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Banda alikuwa na utata kwenye usajili wake na Simba huku akidaiwa kuwa alisaini kwenye timu hiyo ya Msimbazi wakati akiwa bado na mkataba na Coastal Union na timu zote zilipeleka jina la mchezaji huyo kwenye usajili wake lakini aliidhinishwa kuichezea Simba.
Hata hivyo, TFF haijawahi kutangaza adhabu ya beki huyo, bali mwenyewe ameliambia Championi kuwa amefungiwa michezo miwili.
Alianza kwa kuukosa mchezo dhidi ya Coastal Union uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam juzi na timu hizo kutoka sare ya mabao 2-2 na sasa ataukosa na mchezo ujao dhidi ya Polisi Moro.

Banda alisema licha ya TFF kuweka bayana kuwa ataitumukia Simba katika msimu huu, pia shirikisho hilo limempa adhabu ya kumfungia mechi mbili.

“Sitakuwepo uwanjani wakati timu yangu ikicheza na Polisi Moro kutokana na adhabu ambayo inanilazimu kuwa nje kwa michezo miwili niliyopewa na TFF, lakini hii ndiyo itakuwa mechi ya pili baada ya awali kuikosa Coastal Union wikiendi iliyopita,” alisema Banda.

Banda amejiunga na Simba akitokea Coastal Union ya Tanga ambayo alicheza kwa mafanikio msimu uliopita.

Hata hivyo alishindwa kuonyesha cheche zake katika mechi za majaribio kujiandaa na msimu mpya.

Lakini Banda ameahidi kuwa taratibu ataanza kurejea kwenye kiwango chake na kuonyesha uwezo wa juu kama ilivyokuwa msimu uliopita.

No comments

Powered by Blogger.