Header Ads

Mambo manne magumu Bunge Maalumu la Katiba

            Dodoma. Bunge Maalumu la Katiba limebaini mambo manne magumu ambayo yameonekana kuzua mivutano isiyo na mwafaka katika vikao vya kamati zake.

Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta ameyataja mambo hayo kuwa ni mahakama ya kadhi, uraia pacha, muundo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano na kamati ya pamoja ya fedha ya muungano.
Sitta alisema taarifa kutoka kwa wenyeviti wa kamati za Bunge hilo zinathibitisha kuwapo kwa mijadala mikali na mivutano, jambo ambalo limeisukuma Kamati ya Uongozi kuunda kamati maalumu ya watu 10 kuyafanyia kazi mambo hayo.
Akizungumza na waandishi wa habari bungeni mjini hapa jana, Sitta alisema kamati hiyo ndogo itaongozwa na Makamu wake, Samia Suluhu Hassan.
“Kamati hii italeta mapendekezo ambayo yatahitimisha masuala yenye utata kabla ya kufanya uamuzi wa mwisho wa kupiga kura,” alisema Sitta.
Alisema Muundo wa Bunge umeingizwa katika mambo hayo kwa sababu kwa mujibu wa mapendekezo ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, mambo yanayohusu muungano yamepunguzwa kutoka 22 hadi saba.
“Kwa hiyo wakikuta kuwa sura ina mambo hayo wanaahirisha mjadala na kusonga mbele ili wapate ufafanuzi,” alisema Sitta.
Alisema ameagiza ufanyike utaratibu wa kuwaita wataalamu wa juu wa fedha wakiwamo makatibu wakuu kutoka Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Gavana wa Benki Kuu (BoT), kwa ajili ya kupata ushauri wa kitaalamu kutoka kwao... “Wanakuja hapa Jumamosi, kuzungumza na hizi kamati (za Bunge).”
Kuhusu uraia pacha, Sitta alisema suala hilo lina matatizo kutokana utekelezaji wake katika nchi mbalimbali. Alisema wamewaita wataalamu kutoka Idara ya Uhamiaji na Profesa Boniventure Rutinwa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa ajili ya kutoa somo kuhusu suala hilo la uraia pacha.
Alisema pia Bunge limewaalika wataalamu wa sheria akiwamo Profesa Issa Shivji ambao watatoa ushauri wa kitaalamu kuhusu aina ya muundo wa Bunge unaofaa.
Muundo wa Bunge ni moja ya mambo yaliyozua mvutano kwenye kamati kiasi cha kuwagawa wajumbe na tayari baadhi yao wameamua kwamba wataandika maoni ya wachache baada ya kutokubaliana na wenzao.
Katika Kamati Namba Tano, wajumbe waligawanyika na wale wanaotoka upande wa Zanzibar wakitaka muundo wa sasa uendelee, hoja inayopingwa na wajumbe wa Bara wanaotaka muundo ubadilishwe na kuwa na Bunge moja lenye sehemu tatu.

No comments

Powered by Blogger.