Header Ads

Rasimu ya Warioba sasa mifupa mitupu




Mjumbe  wa  Bunge la Katiba Andrew  Chenge(kulia), akifurahia jambo  na wajumbe wenzake, Salehe Pamba (wa pili kushoto),  Adam Malima na Vita Kawawa nje ya ukumbi wa Bunge Mjini Dodoma jana.


Dodoma. Kamati za Bunge Maalumu, zimekamilisha kazi ya kujadili na kuchambua Rasimu ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, huku ikiwa imefanyiwa mabadiliko makubwa tofauti na ilivyokuwa awali.
Wajumbe wanatarajiwa kuanza kukutana kama Bunge zima kuanzia Jumanne ijayo, Septemba 2, 2014 wakati kamati zitakaposoma taarifa zake baada ya kufanya uchambuzi wa sura 15 za Rasimu ya Katiba
kwa zaidi ya wiki tatu, huku yakitarajiwa mabadiliko makubwa.
Mabadiliko yaliyofanywa yameondoa mambo makubwa yaliyokuwa yakiifanya rasimu hiyo kuonekana mpya, hivyo sasa baadhi ya wachambuzi wa mambo wanaiona rasimu kama ‘Katiba ya 1977 iliyofanyiwa marekebisho.’
Mwelekeo wa kubadili karibu misingi yote muhimu iliyojengwa na tume iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba akiwa mwenyekiti, ilianza baada ya kuwekwa kando kwa mfumo wa muungano wa Serikali tatu uliopendekezwa na badala yake kurejea katika muundo wa sasa wa serikali mbili.
Uamuzi huo uliathiri mtiririko na muundo mzima wa sura na ibara za rasimu hiyo, kwani sasa wajumbe wa Bunge Maalumu walilazimika kutengeneza Katiba yenye mwelekeo wa serikali mbili na siyo tatu tena zilizokuwa zimependekezwa na tume.
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad aliwahi kuliambia gazeti hili kwamba mwelekeo wa uchambuzi wa rasimu kwa sura hizo 15, lazima ufuate kile ambacho kamati zilikiamua katika uchambuzi wa awali wa sura ya kwanza na ya sita.
Miongoni mwa mambo ambayo yameachwa baada ya kurejesha mfumo wa serikali mbili ni muundo wa uongozi wa juu wa nchi hususan nafasi ya Makamu wa Rais, muundo wa Bunge la Jamhuri, kupunguzwa mamlaka ya Rais, uwajibikaji na uwajibishwaji wa wabunge na ukomo wa ubunge.
Kadhalika, habari kutoka ndani ya kamati zilisema suala la kuwekwa kwa maadili ya uongozi kwenye Katiba nalo lilizua mjadala mkali kutokana na baadhi ya wajumbe kutaka liondolewe kwa maelezo kwamba linapaswa litajwe kwenye sheria na siyo Katiba.
Mambo ya muungano
Miongoni mwa mambo ambayo kuna kila dalili kwamba yatabadilika ni Bunge Maalumu kuongeza mambo ya muungano kutoka saba yaliyopendekezwa na tume na huenda idadi yake ikazidi 22 yaliyomo kwenye Katiba ya sasa.
 Uchunguzi wa gazeti hili uliofanywa katika baadhi ya kamati za Bunge hilo na kuthibitishwa na baadhi ya wenyeviti wake, umebaini kuwa yapo mapendekezo ya mambo ya muungano kuongezwa, tofauti na mtazamo wa awali kwamba yangepungua kama moja ya njia za kuondoa kero za muungano.
Tume ya Jaji Warioba ilipendekeza mambo saba tu kwenye orodha ya muungano chini ya mfumo wa Serikali tatu, mfumo ambao hata hivyo ni dhahiri umeshawekwa kando na Bunge Maalumu na kurejesha muundo wa serikali mbili.
SOURCE: MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.