Header Ads

Mgawanyo wa mapato watikisa Bunge Maalumu


Samwel Sitta akifafanua jambo 
 
Dodoma. Hoja kuhusu mgawanyo wa mapato ya muungano imeendelea kulitikisa Bunge Maalumu la Katiba na jana watendaji wakuu wa wizara za fedha wa muungano na Zanzibar pamoja na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu walitua Dodoma kuweka mambo sawa.

Vigogo hao wa fedha jana walikutana na baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu, kujaribu kupata mwafaka wa jinsi suala hilo litakavyowekwa kwenye Katiba Mpya.
Bunge la Katiba limelazimika kuwaita Dodoma watendaji hao ili kusaidia kukwamua mgogoro wa mapato ya muungano, ambao uliwagawa wajumbe wa kamati za Bunge hilo wakati wa mjadala wa sura ya 14 kwenye Rasimu ya Katiba.
Pamoja na Profesa Ndulu, wengine waliokuwapo ni Katibu Mkuu Hazina, Dk Servacius Likwelile na mwenzake kutoka Zanzibar, Mussa Omar ambao walikuwa na kibarua kigumu cha kupunguza ufa uliowatenga wajumbe wa Bunge hilo katika misingi ya Ubara na Uzanzibari.
Sura ya 14 ya rasimu ndiyo inayozungumzia masuala ya mapato ya muungano na mgawanyo wake.
Suala la mgawanyo wa mapato ni moja ya mambo manne magumu yaliyosababisha mvutano mkubwa katika kamati za Bunge hilo kiasi cha kusababisha Kamati ya Uongozi ya Bunge Maalumu kuunda kamati ndogo ili kulifanyia kazi.
Kutokana na kusababisha mivutano hiyo, Kamati Namba Moja iliamua kutolijadili kabisa suala hilo na badala yake, kuomba uongozi wa Bunge uwalete watendaji wakuu wa masuala ya fedha ili watoe mwongozo wa kuwawezesha wajumbe kujadili na kupata mwafaka wa jinsi fedha zitakavyoweza kusimamiwa na kugawanywa. Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye pia ni Naibu Waziri - Ofisi ya Makamu wa Rais, Ummy Mwalimu alisema walishindwa kupigia kura sura ya 14 baada ya kuona ina utata.
“Ni kweli hatukupigia kura sura ya 14 pekee, tuliona ina utata mkubwa ambao unahitaji ufafanuzi wa kina na bila shaka baada ya semina ya leo (jana) tutakutana kufanya uamuzi,” alisema Mwalimu.
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Hamis Hamad alisema: “Kamati zote zimemaliza kazi, isipokuwa Namba Moja haikupigia kura sura ya 14 wakitaka ufafanuzi wa kitaalamu, ndiyo maana tumewaleta wataalamu leo.”
Alisema pamoja na kupigia kura sura hiyo, lakini hata kamati nyingine zilionekana kutoelewa vizuri sura hiyo, hivyo ujio wa wataalamu ulilenga kuwawezesha kujadili sehemu hiyo ya Katiba wakiwa na uelewa mpana.
Habari zinasema sura iliyojitokeza kwenye mijadala ya kamati zote 12 ilihamia kwenye semina hiyo, ambako ufa ulidhihirika baina ya wajumbe wa pande hizo mbili za muungano, lakini watendaji hao kwa kushirikiana na wataalamu wengine walifanikiwa kutoa mwelekeo wenye matumaini.
SOURCE: MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.