ISIS inavyotesa Wayazidi nchini Iraq
Wapiganaji wa kundi la kigaidi la ISIS
wameyafanya maisha ya jamii ya Yazidi kuwa mabaya kwa kuwa wamelazimika
kuyakimbia makazi yao.
Irbil, Iraq. Kipi kibaya zaidi: Kuwa mkimbizi au kubaki nchini mwako ufe kwa njaa na kiu?
Ni swali gumu lisilojibika kwa urahisi. Lakini pia
ni vigumu kuipata picha halisi ya maisha ya raia wa Iraq wa jamii ya
Yazidi ambayo imekuwa ikiyapitia katika kipindi cha wiki mbili baada ya
kuwakimbia wapiganaji wa kikundi cha Islamic State of Iraq and Syria (
ISIS).
“Kwa macho yangu nilimshuhudia mbwa akila mzoga wa
binadamu,” Tariq kutoka jamii ya Kiyazidi alikiambia kituo cha
televisheni cha CNN.
Alisema: “Huu siyo mgogoro. Ni maafa.”
Inapofika usiku, kwa mbali huona mwanga wa taa
kutoka katika mji walioukimbia. Wapo juu ya mlima unaowawezesha kuziona
vyema nyumba zao, lakini hali ilivyo hawajui kama wataweza tena kurejea
huko.
Mlima ambao wamejifadhi kwa sasa, upo karibu na
mpaka wa Syria. Kama isingekuwa machafuko nchini humo, huenda ingekuwa
kimbilio la Wairaq hawa lakini usalama sasa ni kubakia hapo walipo.
Wanachemsha chai katika kopo dogo, hivyo inawalazimu kurudia mara nyingi ili walau kila mmoja apate kitu cha moto tumboni.
Jua linapochomoza, sauti za ndege za kivita
huunguruma juu ya vichwa vyao. Mawazoni mwao hudhani wakati wowote
zitadondosha misaada ya chakula na maji, lakini mwishowe muungurumo huo
hupotea na kurudi tena baadaye.
Siyo ndege za misaada kama wanavyodhani, bali zipo
katika doria ya kulinda mali za wawekezaji katika miji mbalimbali
nchini humo.
Inaelezwa kuwa ndege hizo ni za ulinzi wa mji wa
Irbil ambao una miradi mingi ya wawekezaji kutoka nchi za Magharibi
pamoja na hoteli za kifahari.
Katika mazingira ya nyuzi joto 45.7, wengi wameanza kuchoshwa na njaa na maji ya kunywa yamewaishia.
source: Mwananchi
source: Mwananchi
Post a Comment