Header Ads

BIASHARA HARAMU YA WATOTO: Serikali yatoa saa 48 kuhakiki wageni



 http://www.ippmedia.com/media/picture/large/Gama-Moshi----October25-2014(1).jpg
                                     Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama


Serikali mkoani Kilimanjaro, imetoa saa 48 kwa maofisa watendaji kata, vijiji na mitaa, kufanya zoezi maalum la uhakiki wa wageni, wanaodaiwa kutumia mwavuli wa dini kuendesha biashara haramu ya wizi wa watoto.
 
Agizo hilo limekuja siku chache baada ya kugundulika mahali walipofichwa watoto 29, wanaodaiwa kupotea kwenye mazingira ya kutatanisha katika mikoa 13 nchini na  kuhifadhiwa kwenye makazi hayo kinyume cha sheria za nchi.
 
Mkuu wa mkoa huo, Leonidas Gama, akizungumza na NIPASHE Jumapili, kuhusiana na uhakiki huo, alisema unalenga kusaidia kupunguza hofu na hasira ya umma kuhusiana na usalama wa watoto hao; na mahali wanakopelekwa baada ya kupatiwa mafunzo maalum ya kujihami pamoja na elimu ya dini.
 
“Nimeagiza ndani ya saa 48, kila mtendaji kwenye ngazi za vijiji, mitaa na kata, wawe wamewatambua watu wote na kuwasilisha taarifa za siri kwa wakuu wa wilaya zao. Baada ya zoezi hilo nitatoa taarifa rasmi kwa umma, Jumanne ya wiki ijayo kuhusu hali ya usalama katika mkoa wetu,” alisema Gama.
 
Watoto walio okolewa hadi sasa, baada ya kugunduliwa kwa matukio hayo ni wenye umri wa miaka miwili hadi 16, ambao walikutwa wamehifadhiwa kwenye nyumba moja, iliyopo karibu na uwanja wa Mandela, Kata ya Pasua, Manispaa ya Moshi, mali ya mfanyabiashara wa nguo nchini Kenya, Abdelnasir Abdurahaman, maarufu kama Karata (33), huku watoto wengine 11, wakiokolewa pia katika kituo cha UMM Sakhail, kilichopo Lyamungo, Wilaya ya Hai.
 
Hata hivyo, kwa mujibu wa Tangazo la Serikali namba 280 la mwaka 2002, pamoja na kifungu cha 353 cha Sheria ya Elimu, iliyofanyiwa marejeo mwaka 2002; mzazi yeyote au mlezi atakayeshindwa kuhakikisha mwanae anapata elimu ya msingi kwa wakati husika, atashtakiwa, kulipishwa faini au kupata adhabu ya kifungo, iwapo atashindwa kutimiza matakwa ya sheria hiyo.
 
Kufuatia taharuki hiyo kuikumba mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara, Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Ernest Mangu, juzi alilazimika kukutana na kutetea kwa zaidi ya saa sita na timu ya makachero wa makao makuu ya jeshi hilo pamoja na maofisa wake wa mkoa wa Kilimanjaro, ikiwa ni siku tano baada ya kukamatwa kwa wafanyabiashara wanaodaiwa kuwahifadhi watoto kutoka mikoa mbalimbali nchini.
 
Alipoulizwa iwapo watoto hao, wanatokea mikoa ipi ya Tanzania; Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Geofrey Kamwela, alisema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa watoto hao ni wakazi wa mikoa ya Tanga, Mtwara, Mbeya, Tabora, Manyara, Arusha, Kagera, Mara, Kilimanjaro, Dodoma na Shinyanga.
 
 
CHANZO: NIPASHE

No comments

Powered by Blogger.